Baada 
 ya uamuzi wa kuwafukuza vyuo walimu wanne waliokuwa kwenye mafunzo ya 
vitendo katika Shule ya Sekondari ya Kutwa ya Mbeya (Mbeya Day), 
serikali imesema vyuo husika vinaweza kushauri adhabu mbadala iwapo 
vitajiridhisha kuwepo kwa mazingira tofauti na yaliyozingatiwa kwenye 
uamuzi wa kuwafukuza vyuo.
Waziri
 wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce 
Ndalichako alisema hayo juzi alipozungumza na waandishi wa habari mkoani
 Mbeya alikokuwa katika ziara kwenye shule mbalimbali mkoani humo.
Profesa
 Ndalichako alisema uamuzi uliochukuliwa na ofisi yake ulizingatia 
sheria ndogo zilizotungwa katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Udsm) 
zinazoainisha makosa yanayoweza kumfukuzisha chuo mwanafunzi.
Hata
 hivyo, alisema uamuzi uliochukuliwa unaweza kutazamwa upya na vyuo 
husika iwapo uzito uliochukuliwa na wizara utaonekana kuwa katika 
mazingira na uhalisia wa tukio husika.
Walimu
 wanne waliokuwa kwa vitendo katika shule ya Mbeya Day walifukuzwa vyuo 
baada ya uamuzi wa serikali kutokana na kuhusika kumpiga mwanafunzi 
Sebastain Chinguku vibao, mateke na fimbo kwa ukatili Septemba 28 mwaka 
huu shuleni humo.
Walimu hao walibainika baada ya kipande cha video kusambazwa katika mitandao ya kijamii hivi karibuni. 
Waliohusika
 na vyuo walivyokuwa wakisoma ni Frank Msigwa (anayedaiwa kumpiga zaidi 
mwanafunzi makofi kichwani), John Deo na Sante Gwamaka wote wa 
DUCE-UDSM, na Evans Sanga wa Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Mwalimu 
Nyerere.
Akijibu
 swali la idadi ipi ya viboko inastahili kutolewa kama adhabu kwa 
mwanafunzi anayekwenda kinyume na maelekezo ya shule yake, Profesa 
Ndalichako alisema binafsi asingependa mwanafunzi achapwe hata kiboko 
kimoja lakini hilo linawezekana pale wanafunzi watakapozingatia maadili.
“Adhabu
 yoyote kwa mwanafunzi inatolewa pale anapokuwa amekwenda kinyume na 
maadili ya shule yake. Kama wanafunzi wote watazingatia maadili sidhani 
kama kuna mwalimu atakayempiga mwanafunzi hata kiboko kimoja. Haya yote 
yanatokea kutokana na wanafunzi kukosa nidhamu,” alisisitiza Ndalichako.
Aliwasihi
 wanafunzi kuzingatia maadili ya shule yao, akisema ndiyo njia pekee ya 
kuwawezesha kuishi vyema na walimu wao na pia kufanya vyema kitaaluma na
 kuwasihi wazazi kuwafundisha watoto wao nidhamu ya kuwaheshimu watu 
wote, akisema malezi hayo yatawapunguzia walimu adha ya kuishi na 
wanafunzi watukutu ambao kimsingi wanazorotesha utendaji kazi wao.
Sign up here with your email

ConversionConversion EmoticonEmoticon