Vilio
 vya furaha kutoka kwa ndugu, jamaa na marafiki, vimetawala katika 
Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam 
jana, baada ya kuwasili kwa madereva 10 wa Tanzania waliotekwa na 
kunusurika nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Madereva
 hao waliwasili katika uwanja huo saa 9 alasiri, wakitoka Kigali, Rwanda
 kwa ndege ya Shirika la Ndege la Rwanda na kukutana na familia zao kwa 
mara ya kwanza baada ya kuokolewa.
Wakiwa
 uwanja wa ndege, walizungumza na waandishi wa habari na kueleza namna 
walivyotekwa na waasi waliovalia sare za jeshi zisizofanana na 
walivyosafirishwa zaidi ya kilometa 50 porini usiku na mchana, 
wakitembea kwa magoti na kupoteza tumaini la kupona huku baadhi 
wakifanikiwa kutoroka na wengine kuokolewa.
Kabla
 ya kuwasili kwa madereva hao, ndugu hao walikusanyika uwanjani hapo 
wakiwa na shauku ya kukutana na madereva hao ambao Septemba 14, mwaka 
huu, walikumbwa na kadhia ya kutekwa na kundi la wanamgambo huku magari 
waliyokuwa nayo yakichomwa moto na hatma yao kutojulikana.
Hata
 hivyo, kutokana na juhudi za Serikali ya DRC na Tanzania, madereva hao 
walifanikiwa kuokolewa na kupatiwa matibabu ambapo jana walirejea nchini
 rasmi.
Baada
 ya madereva hao kumaliza kuzungumza na waandishi wa habari, walitoka 
nje kwenda kuonana na ndugu zao waliokuwa wamekusanywa pembeni, lakini 
walipowaona tu walishindwa kujizuia na kuwakimbilia madereva hao ambao 
nao waliwakimbilia huku wakilia na kutamka maneno ya kumshukuru Mungu 
kwa kuonana tena.
Baadhi
 ya familia ziliambatana na watoto wa madereva hao, ambao katika hali ya
 kutia simanzi baada ya kuwaona wazazi wao, waliangua kilio kwa sauti 
huku wakiwaita baba zao na kuwakumbatia kwa furaha.
Madereva
 waliookolewa kutoka Tanzania na waliowasili jana ni Kumbuka Selemani, 
Hussein Mohammed, Bakari Nassoro, Issa Omary, Amdani Zarafi, Adam James,
 Mbwana Said, Ali Juma, Athuman Fadhil na Amis Mshana.
Familia za madereva zazungumza 
Mke
 wa dereva Ali Juma, Jamila Ali, alisema anamshukuru Mungu kwa kuonana 
tena na mumewe, jambo ambalo hakulitarajia kwani baada ya kupewa taarifa
 za kutekwa kwake, walikata tamaa ya kumuona tena. Pia alizishukuru 
Serikali zote mbili kwa juhudi za haraka, walizochukua baada ya kupata 
taarifa ya kutekwa kwa mumewe na wenzake.
“Mimi
 nilipata taarifa kutoka kwa mwanangu mkubwa aliyenisihi nimpigie simu 
baba yake, lakini baada ya kupiga simu ilikuwa ikipokewa na kuwekwa 
pembeni bila mtu kuongea, lakini nilisikia watu wakiongea kwa lugha ya 
kifaransa mpaka nikamaliza vocha yangu ya Sh 10,000,” alisema.
Alisema
 wakati akipiga simu hiyo, alikuwa hafahamu chochote kuhusu kutekwa kwa 
mumewe, ila baadaye alisikia kwenye taarifa ya habari, ndipo alipotambua
 kuwa na mumewe yupo miongoni mwa madereva waliotekwa kutokana na 
kampuni iliyotajwa ambao ni Simba Logistics.
Mariam
 Ayoub ambaye ni mke wa Mbwana Said, alisema anamshukuru Mungu baada ya 
mumewe kurejea salama na kwamba siku ya jana ni ya furaha kwake na 
familia yake. 
Alisema
 tangu apate taarifa za kutekwa kwa mumewe kupitia taarifa ya habari 
hakuweza kula, wala kulala usingizi huku akiwa na mtoto mdogo wa mwaka 
mmoja na nusu.
 “Leo nina furaha kubwa wala siwezi kuelezea zaidi,” alisema huku akilia.
Naye
 dada wa Bakari Nassoro, Halima Juma ambaye alikuwa akielezea furaha ya 
kuonana na ndugu huku akilia, alisema familia yake ilishakata tamaa ya 
kumuona tena ndugu yao huyo kutokana na simulizi za kutisha, walizokuwa 
wakihadithiwa kuhusu waasi wa DRC. 
Baada
 ya kuonana na familia zao, madereva hao walipiga picha ya kumbukumbu na
 kisha kuondoka uwanjani hapo kila dereva na familia yake.
Madereva wasimulia 
Awali
 wakati akisimulia kama sinema juu ya kilichowapata wakati wakitekwa, 
Kumbuka Selemani, alisema siku hiyo ya Septemba 14, mwaka huu katika 
eneo la Namoya Jimbo la Kivu Kusini mwa nchi ya DRC, madereva hao 
walitoka kushusha mzigo wa saruji kilometa 12 kutoka eneo walilotekewa.
Alisema
 mara baada ya kushusha mzigo huo wakati wakirejea, walikuwa 
wakiongozana na magari mengine ya kampuni hiyo ya Simba Logistics yeye 
akiwa dereva wa gari namba nane.
Alisema
 wakati akikaribia eneo la Kivu, ghafla alisimamishwa na mtu aliyekuwa 
amebeba silaha nzito huku amevaa mavazi ya jeshi yasiyoeleweka, kwa 
maana ya kuchanganywa na kumtaka ashuke kwenye gari hilo na amkabidhi 
kila kitu, ikiwemo hati yake ya kusafiria na kadi ya gari.
“Wakati
 nimeshashuka niko chini namkabidhi vitu vyangu, mara lilitokea gari la 
tisa ambalo baada ya kumuona yule mwanajeshi, lilisimama na kuanza 
kugeuza kwa maana ya kukimbia. Ndipo yule askari akaachana na mimi 
akaanza kulirushia risasi lile gari lililokuwa linaendelea kugeuza,” alisimulia.
Alisema
 risasi zile kwa bahati zilipiga kwenye kioo cha pembeni cha lori 
lingine la 10 lililokuwa linalokuja ambalo nalo baada ya kuona hali ile 
liligeuza. “Mimi nilipoona ameelekeza mawazo yake kwenye yale magari nikapata upenyo na kukimbilia porini.”
Alisema
 aliingia msituni na kuanza kutembea umbali mrefu akitafuta kujiokoa 
hadi alipoona kikosi kingine cha polisi ambacho alilazimika kukichunguza
 kwanza ili kujua kama ni wale watekaji au askari halali wa nchi hiyo.
Alisema
 alibaini kuwa ni askari halali kutokana na mavazi yao kuwa ya kawaida 
ya kipolisi bila kuchanganywa ndipo alipojitokeza na kujisalimisha kwa 
kunyoosha mikono juu. Askari wale walimchukua na kumhoji na kisha 
kumpatia huduma za kawaida ikiwemo chakula.
“Wakati
 najiandaa kupanda pikipiki kwenda kula nikashangaa namuona na mwenzangu
 (Mshana) ambaye naye alitoroka nikaunganishwa naye,” alisema.
Kwa
 upande wake Mshana, alisema naye alisimamishwa na kuamriwa ashuke 
kwenye gari na kukabidhi kila kitu ikiwemo hati yake ya kusafiria na 
simu. Aliunganishwa na wenzake aliowakuta tayari wametekwa na kuongozwa 
kuelekea porini huku wakiwa wamefungwa mikono.
Alisema
 katika msafara huo, mmoja wa askari alitangulia mbele na wengine 
walifuatia nyuma na kuongozwa kwenye pori zito ambalo wakati mwingine 
walilazimika kutembea kwa magoti kwani haikuwezekana kutembea huku 
umesimama.
“Tulipotembea
 kama kilometa 13 ikabidi nimwambie mwenzangu (Athuman Fadhil) kwamba 
tutafute njia ya kujiokoa. Hata hivyo alinijibu kwamba kuwa yeye hawezi 
kwa kuwa amevaa nguo inayomtambulisha zaidi endapo akitoroka itajulikana
 na wenzetu watapata shida,” alisema.
Alisema
 walitembea mbele kidogo ndipo alipobaini umbali kidogo kati yake na 
askari ambapo pembeni yake kulikuwa na kinjia cha kujipenyeza ndipo 
alipoamua kutambaa kwa magoti na kujipenyeza kwenye kinjia hicho na 
kufanikiwa kujificha bila kuonekana.
Alisema
 mara baada ya wenzake kupita alianza safari kwenye pori hilo bila kujua
 anakokwenda mpaka alipofanikiwa kukutana na kikosi cha Polisi ambacho 
kilimchukua na kumpeleka sehemu salama.
Athuman
 Fadhili ambaye alitekwa hadi kuokolewa na majeshi ya DRC, alisema baada
 ya mwenzake kutoroka alipata matumaini kuwa atasaidia kuwaletea msaada 
hivyo waliendelea na safari kama kilometa 30 zaidi kwenye msitu huo 
mnene.
Alisema
 katika safari hiyo ya mateso ya siku mbili walitembea usiku na mchana 
huku wakichanwachanwa na miba, walifika kwenye eneo la kijiji ambacho 
hata hivyo kilikuwa na nyumba chache, wakaamriwa watembee kwa kutambaa 
ili wasionekane na wanakijiji hao.
Baada
 ya kilometa tano kutoka kwenye hicho kijiji walifika kwenye makazi ya 
muda ya watekaji hao na kukutana na mkubwa wao aliyejitambulisha kama 
Shehe Hassan aliyeamuru wapewe maji na kuanza kuwahoji majina yao 
kupitia hati zao za kusafiria na kutaka kujua kuhusu familia zao.
Walibeba mizigo ya waasi 
Alisema
 wakiwa katika eneo hilo, mmoja wa viongozi wa watekaji hao aliyekuwa 
akizungumza kwa simu na bosi wao mwingine alitoa taarifa kuwa majeshi ya
 DRC yanawafuatilia hivyo wanatakiwa kujihadhari.
Baada
 ya mahojiano hayo walipewa chakula na maji na kisha giza lilipoingia 
walitafutiwa eneo la kulala ambalo ni hema lililowekewa turubai. Alisema
 majira ya saa sita au saa saba usiku huku mvua kubwa ikiwa inanyesha, 
waliamshwa na kutakiwa kuendelea na safari kwa kuwa hali ya usalama 
katika eneo hilo ni tata kutokana na majeshi ya DRC kuzidi kuwakaribia.
“Tulikuwa
 tumechoka sana kutokana na kubeba mizigo yetu na yao safari nzima 
lakini tulilazimika kutembea tu. Ilifikia mahali tulitamani kupigwa hata
 risasi ili tupumzike na kuondokana na mateso tuliyokuwa tunayapata,” alisema Fadhili.
Walitaka dola 4,000 kutoka kwa Dewji 
Alisema
 wakati wakiendelea kutembea, viongozi wa watekaji hao waliendelea 
kuwasiliana njia nzima na bosi wa Simba Logistics, Azim Dewji na kumpa 
saa 24 awe ametoa dola za Marekani 4,000 kwa kila dereva ili waachiwe 
huru.
“Lakini
 baadaye wao wenyewe wakaanza kubishana juu ya namna ya kuzipata fedha 
hizo kutokana na hali halisi ya msitu huo. Wakaambizana fedha hizo 
zipelekwe kupitia helikopta ya kampuni walikoshushia mzigo wa saruji na 
madereva hao wapepee bendera kuonesha wako salama na fedha hizo 
zidondoshwe,” alifafanua.
Alisema
 walitembea tena umbali kidogo ndipo waliposimama na kupewa chakula aina
 ya ugali wa mhogo uliokuwa umejaa michanga pamoja na mboga za majani 
wasiyoyajua na kulazimika kula tu kwa kuwa walikuwa na njaa.
Fadhil
 alisema waliendelea kubaki katika eneo hilo kwa muda, ndipo watekaji 
hao walipomtuma kijana wao akanunua unga mjini, baada ya muda alirejea 
akiwa anatweta na kuwataarifu kwa taharuki kuwa majeshi ya DRC 
yamekaribia eneo hilo.
Madereva wagawanywa kwa waasi
Kutokana
 na taharuki ya viongozi hao, kila mtekaji alipewa madereva wawili mpaka
 watatu awaongoze na kuanza kukimbia huku watekaji hao wakiwa 
wametangulia mbele.
“Walionesha
 kuchanganyikiwa kwa kweli wakaanza kutufokea huku wametushikia mitutu 
ya bunduki na kila kundi likaenda upande wake. Kwa kuwa wao ndio 
waliotangulia, tukaanza kutoroka mmoja mmoja mpaka kwenye kundi letu 
tukabaki wawili mimi na Issa,” alisema.
Alisema
 baada ya kubakia wawili wakaamua pia na wao watoroke kwani hali ilikuwa
 tete hivyo wakajitosa msituni na kuanza kukimbia hadi waliposikia sauti
 za maaskari wa DRC zikiwaita.
“Tulisikia
 wakituita kwa lafudhi yao ya kikongo, watanzania kuya (kuja) watanzania
 kuya (kuja) jitokezeni sisi ni jeshi la DRC tumewaokoa. Sikuamini 
masikio yangu tulijitokeza na kupewa msaada haraka,” alisema.
Dewji, Serikali ya Tanzania na Congo wazungumza 
Kwa
 upande wake, Dewji alilishukuru jeshi la DRC na Serikali ya Tanzania 
kwa kuwa naye bega kwa bega katika harakati za kuwaokoa madereva hao na 
kubainisha kuwa katika tukio hilo, magari ya kampuni yake ya Simba manne
 yalichomwa moto na hivyo kupata hasara ya Sh milioni 600.
Alisema
 alikuwa akiwasiliana na waasi hao kila mara wakimtaka atoe fedha hizo 
ambazo alikuwa tayari kuzitoa lakini alionywa na jeshi la DRC kuwa 
endapo atazitoa atawajengea tabia ya utekaji zaidi wanajeshi hao.
Aidha,
 Dewji alisema Serikali ya DRC imemuahidi kuwa itaendelea kuweka usalama
 kwa wafanyabiashara wa malori nchini humo na kumhakikishia ulinzi wa 
doria kila kampuni hiyo itakaposafirisha mizigo yake nchini.
 “Hiki
 kilichotokea ni bahati mbaya, tutaendelea na biashara lakini kwa 
tahadhari. Biashara yangu inagusa watu wengi si kampuni yangu pekee 
endapo nitasitisha wengi wataathirika,” alisisitiza.
Balozi
 wa DRC nchini, Jean Piorre Mutamba, alisema tukio hilo limemshtua na 
kumpa wakati mgumu, hasa ikizingatiwa kuwa ni balozi mpya aliyewasili 
nchini hivi karibuni, hivyo alitumia fikra zake zote ili kuhakikisha 
madereva hao wanaokolewa. 
Aliwataka
 madereva hao kuhakikisha wanawasiliana na ubalozi wa DRC kabla ya 
kuanza safari ili kuwawekea mazingira ya usalama zaidi na kuwafuatilia.
Kwa
 upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika 
Mashariki, Susan Kolimba, aliwahakikishia madereva hao kwamba tukio hilo
 ni la bahati mbaya na kwamba Serikali ya Tanzania itaendelea kuwalinda 
wananchi wake wanaofanya kazi nje ya nchi.
“DRC
 ni nchi rafiki na tumekuwa tukifanya nao kazi nyingi. Nina imani tukio 
hili haliwezi kuvunja uhusiano wetu kwani serikali zote mbili zimefanya 
jitihada kubwa za kuwaokoa madereva hao,” alisisitiza.
Sign up here with your email





ConversionConversion EmoticonEmoticon