Kipa Yanga nje wiki mbili

GOLIKIPA BENO KAKOLANYA.

WAKATI mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ukitarajiwa kuanza Jumamosi juma hili, wachezaji wawili wa Yanga huenda wakawa nje ya uwanja kwa wiki mbili zaidi kutokana na majeraha waliyoyapata mazoezini.
Wachezaji hao ni golikipa Beno Kakolanya na mshambuliaji Matheo Anthony.

Akizungumza na Nipashe jana, Meneja wa timu hiyo, Hafidhi Saleh, alisema golikipa Kakolanya ameumia nyonga huku Matheo akiwa na maumivu ya mguu.

"Tuna majeruhi wawili tu, Kakolanya na Matheo, hawa wote kwa sasa hawafanyi mazoezi kutokana na kuwa nje wakiuguza majeraha yao, lakini wengine wapo vizuri," alisema Saleh.

Alisema kwa sasa wanafanya mazoezi mara mbili kwa siku kwenye uwanja wa Chuo cha Polisi, Kurasini jijini Dar es Salaam.

"Programu hii ya mazoezi itaendelea mpaka tutakapoanza mzunguko wa pili, ambapo itabadilika kulingana na majukumu ya timu," alisema.

Alisema baada ya kuanza mechi za mzunguko wa pili, ratiba ya mazoezi itakuwa ikibadilika kulingana na siku za mechi zao.
Yanga itaanza mzunguko wa pili kwa kucheza na JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Previous
Next Post »

COMMUNITY HELP